Halmashauri ya Mji Njombe imetoa kiasi cha Shilingi milioni mia saba laki tisa kwa vikundi 72 vya kiuchumi vya Wanawake, Vijana na Walemavu kwa kipindi cha robo ya kwanza ya mwaka 2020/2021.
Kiasi hicho cha fedha kinatokana na makusanyo ya mapato ya ndani ambapo kiasi cha Shilingi milioni 120 zimechangiwa, huku kiasi kilichosalia ikiwi ni fedha za marejesho.
Akizungumza wakati wa hafla ya kukabidhi mfano wa hundi kwa vikundi hivyo, Mkuu wa Mkoa wa Njombe Mhandisi Marwa Rubirya amevitaka vikundi hivyo kufanya matumizi sahihi ya mikopo hiyo ili kuwa endelevu na kufanya marejesho kwa wakati jambo litakaloviwezesha vikundi vingine kukopa.
“Mikopo hii ikatumike kwa malengo yaliyokusudiwa. Sio mnatumia fedha hizi kama kikundi mkifika kule mnagawana.Mwingine anaenda kununua baiskeli mwingine anaenda kulipa ada ya shule.Hayo sio malengo ya mkopo huu.”
Awali akiwasilisha taarifa ya hali ya utoaji wa mikopo katika Halmashauri Afisa Maendeleo ya Jamii Enembora Lema amesema kuwa Hali ya utoaji wa mikopo katika Halmashauri imeendelea kuimarika kila wakati kwani kwa mwaka wa fedha 2018/2019 Halmashauri ilitoa TSH. 375,733,00, Mwaka 2019/2020 ilitoa TSH. 676,300,000 na Mwaka 2020/2021 kwa robo ya kwanza pekee Halmashauri imeanza kwa kutoa TSH 700,900,000/=
Kwa upande wao mwakilishi kutoka kundi la walemavu na wanawake wamesema kuwa ni vyema wanavikundi kutumia fedha hizo kuchochea shughuli za maendeleo jambo litakalopelekea kufanya marejesho kwa wakati.
“Tukisema tuchepushe kidogo hii fedha marejesho yatatushinda.Tutaanza kulalamika fedha ya Halmashauri inamkosi kumbe mkosi ni sisi wenyewe.”Alisema Mwakilishi wa Wanawake.
Aggrey Chatanda ni Mwakilishi kutoka Kundi la vijana amesema kuwa fedha hizo zitakwenda kuongezea nguvu kwenye mradi wa nyuki ambao tayari umeanza.
Utaratibu wa Utoaji wa mikopo bila riba kwa vikundi vya Wanawake,Vijana na Wenye ulemavu ulianzishwa ili wanufaika waweze kupata mitaji na kufanya uwekezaji katika shughuli za kiuchumi, Mathalani katika Kilimo,Ufugaji,Uvuvi na kuanzisha viwanda vidogo vidogo na hatimaye kuweza kuboresha Maisha kuanzia ngazi ya Familia,Jamii na Taifa.
Ofisi yetu inapatikana barabara ya Njombe-Songea mtaa wa Mjimwema.
Sanduku la Posta: S.L.P 577
Simu ya Mezani: 026-2968833
Simu ya Mkononi: 026-2968833
Barua Pepe: td@njombetc.go.tz
Haki Miliki ©2017 Halmashauri ya Mji Njombe