Mkuu wa Mkoa wa Njombe Mhandisi Marwa Rubirya leo amekabidhiwa vyumba 103 vya madarasa katika Wilaya ya Njombe ambavyo vyumba hivyo vimejengwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Njombe, Halmashauri ya Mji Makambako na Halmashauri ya Mji Njombe ambapo makabidhiano hayo yamefanyika katika Shule ya Sekondari Mpechi kwa kukabidhiwa vyumba 05 vya madarasa ikiwa ni ishara ya makabidhiano hayo Kiwilaya.
Akizungumza wakati akisoma taarifa ya makabidhiano, Mkuu wa Wilaya ya Njombe Kissa Gwakisa amesema kuwa katika vyumba 103 vya madarasa vilivyojengwa kwenye Wilaya ya Njombe ujenzi wa vyumba hivyo umekamilika kwa asilimia mia moja na pia vimewekewa samani ikiwa ni viti na meza na amezishukuru kamati za ujenzi kwa namna walivyosimamia miradi hii mpaka kukamilika kwake.
“Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutuletea maendeleo Wananchi wa Tanzania kwa miradi hii mikubwa ya ujenzi wa madarasa. Kipindi cha nyuma tulitumia muda huu kuchangisha wananchi ili kidato cha kwanza waweze kuingia madarasani. Lakini leo hii tumejengewa madarasa na Wananfunzi wa kidato cha kwanza wote wanaingia darasani pasipo kumsumbua Mwananchi na michango.”Alisema Kissa
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Njombe Mhandisi Marwa Rubirya amepongeza hatua iliyofikiwa ya ukamilishaji wa vyumba 103 vya madarasa ambavyo chanzo cha fedha za mradi huo ikiwa ni mapambano dhidi ya UVIKO.
“Pamoja na kazi nzuri tuliyoifanya niwape changamoto katika awamu ya pili ya miradi na hii itakuwa ni sera yetu ya Mkoa kuhakikisha kuwa tunajenga mazingira mazuri ya kazi kwa Waalimu ikiwa ni pamoja na kuwajengea ofisi nzuri. Kila tunapojenga vyumba viwili vya madarasa lazima tujenge ofisi kwa ajili ya Waalimu.”Alisema Mkuu wa Mkoa
Aliendelea kusema “Bado tunataka kujua jinsi fedha hii ilivyotumika. Tumeandaa fomu maalumu itakayosambazwa kwenye kila shule itakayokuwa na mchanganuo wa gharama za fedha zilizotumika katika kila hatua ya ujenzi ikiwa ni kuanzia msingi, kupandisha kuta, kuezeka, kupaua na hatua za umaliziaji. Niwapongeze sana Shule ya Sekondari Mpechi kwa hatua hii ya ujenzi. Madarasa ni mazuri na Milango iliyotumika hapa ni ya kiwango cha juu. Alisema Rubirya.
Aidha Mkuu wa Mkoa ametoa rai kwa wazazi na walezi kuhakikisha kuwa watoto wote waliofaulu kidato cha kwanza kuhakikisha kuwa ifikapo januari 17 watoto wote wanaripoti shuleni kwani madarasa yapo ya kutosha na hakuna sababu ya shule kutoyatumia madarasa mapya kwani yamejngwa kwa sababu hiyo.
Shule ya Sekondari Mpechi ilipatiwa kiasi cha Shilingi milioni 100 ikiwa ni kwa ajili ya ujenzi wa vyumba 5 vya madarasa na samani ambavyo vimekabidhiwa rasmi leo
Ofisi yetu inapatikana barabara ya Njombe-Songea mtaa wa Mjimwema.
Sanduku la Posta: S.L.P 577
Simu ya Mezani: 026-2968833
Simu ya Mkononi: 026-2968833
Barua Pepe: td@njombetc.go.tz
Haki Miliki ©2017 Halmashauri ya Mji Njombe