Juni 16, 2025 – Mkuu wa Mkoa wa Njombe Mhe. Anthony Mtaka ameipongeza Halmashauri ya Mji Njombe kwa kupata hati safi katika taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) kwa mwaka wa fedha 2023/2024.
Akizungumza katika mkutano maalum wa Baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo uliolenga kupokea na kujadili hoja za CAG, Mhe. Mtaka alisema hati safi hiyo ni ishara ya uwajibikaji, uadilifu, na usimamizi mzuri wa rasilimali za umma uliofanyika kwa ushirikiano mkubwa kati ya Waheshimiwa madiwani na menejimenti ya Halmashauri ya Mji Njombe.
Alitumia fursa hiyo kuwapongeza waheshimiwa madiwani ambao wanamaliza kipindi chao cha uongozi baada ya miaka mitano akiwasisisitiza kutembea kifua mbele kwakuwa kazi kubwa iliyofanya na serikali kwenye maeneo yao imefanyika kipindi cha uongozi wao,hivyo wayaseme kwa wananchi.
"Madiwani mmefanya kazi kubwa,kwa kipindi cha miaka mitano, thamani ya fedha kwenye miradi ya maendeleo inaonekana.Mnaondoka mkitambuliwa na Serikali kwa kazi kubwa mliyofanikisha. Menejimenti imejituma na miradi mingi imefanikiwa." Alipongeza. Mhe. Mtaka.
Aidha, alipongeza jitihada za utoaji mikopo ya asilimia 10 kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu na kusisitiza umuhimu wa kuhakikisha mikopo hiyo inarejeshwa ili iweze kuwafikia watu wengi zaidi.
"Kamati ya mikopo ifuatilie marejesho na vijana waambiwe wazi kuwa fursa zipo, waombe mikopo halali badala ya kukimbilia mikopo kandamizi," aliongeza.
Alisisitiza umuhimu wa kumaliza hoja 13 zilizobaki na kuepuka mazingira ya hoja zinazojirudia katika miaka ijayo.Aliwakumbusha viongozi kuwa Halmashauri ya Mji Njombe kama makao makuu ya mkoa, inabeba taswira ya mkoa hivyo ni lazima kuwe na mtazamo mpana wa maendeleo.
Alitoa wito kwa Halmashauri kutafuta maeneo mapya kwa ajili ya kupima na kumiliki ardhi ili kujiandaa na kunufaika na fursa za uwekezaji ikiwemo miradi ya kimkakati kama ujenzi wa reli itakayopita Njombe kutokea Wilaya ya Ludewa unapofanyika uwekezaji mkubwa kwenye madini ya chuma na makaa ya mawe kwenye mradi wa Liganga na Mchuchuma.
Ofisi yetu inapatikana barabara ya Njombe-Songea mtaa wa Mjimwema.
Sanduku la Posta: S.L.P 577
Simu ya Mezani: 026-2968833
Simu ya Mkononi: 026-2968833
Barua Pepe: td@njombetc.go.tz
Haki Miliki ©2017 Halmashauri ya Mji Njombe