Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ameongeza siku 10 na hivyo kufanya jumla ya siku 30 kukamilisha ujenzi wa stendi mpya Mkoani Njombe ifikapo Mei 10 mwaka huu.
Agizo hilo amelitoa leo wakati akihutubia Wananchi wa Mkoa wa Njombe kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika viwanja vya sabasaba Mkoani hapo.
“Wananchi wanalalamika stendi imejengwa miaka mitano haiishi kila siku kuna tatizo gani stendi ya Njombe isimalizike.Sijui nani atanipa majibu na sababu tutatue harakaharaka hapa labda Mkurugenzi unaweza kunisaidia Mkurugenzi wa Njombe njoo unieleze hapa kama si wewe nieleze tatizo ni nini?”
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Njombe Illuminata Mwenda ameeleza kuwa stendi hiyo iliyojengwa kwa awamu ya kwanza na ya pili toka mwaka 2013 hadi mwaka 2015 na awamu ya tatu ambayo waliamua kuvunja mkataba na Mkandarasi Masasi Construction kutokana na kusuasua kwa ujenzi wa stendi hiyo na hivyo kuchelewesha kumalizika kwa mradi huo.
Josephat Kandege ni Naibu Waziri wa TAMISEMI, ambaye yeye amesema kuwa tatizo kubwa ni stendi hiyo kuchukua muda mrefu na anakubaliana na Halmashauri kwa kuvunja mkataba wa kwanza na leo amepata fursa ya kuzungumza na mkandarasi mpya ambaye ameahidi ndani ya siku 20 stendi hiyo itakuwa imekamilika.
Mara baada ya taarifa hizo Rais Magufuli aliamua kuongeza muda wa siku kumi na hivyo kufanya siku 30 kukamilika kwa ujenzi wa stendi hiyo.
“Tunasubiri hizo siku 20 mlizotuahidi na mimi nawaongezea siku kumi jumla 30 stendi ikamilike mpaka tarehe 10 mwezi wa 5 stendi iwe imekamilika kwa kiwango kinachotakiwa” Rais Magufuli
“Kuanzia mwaka 2015 mpaka sasa Njombe inamabadiliko makubwa sana. Hongereni sana Wananjombe hii yote kwa sababu Wananchi wa Njombe ni Wafanyakazi na wanajituma. “Rais Magufuli
Ofisi yetu inapatikana barabara ya Njombe-Songea mtaa wa Mjimwema.
Sanduku la Posta: S.L.P 577
Simu ya Mezani: 026-2968833
Simu ya Mkononi: 026-2968833
Barua Pepe: td@njombetc.go.tz
Haki Miliki ©2017 Halmashauri ya Mji Njombe