Mkuu wa Mkoa wa Njombe Antony Mtaka amezitaka Halmashauri kuwa na mawazo ya kipekee na kibunifu juu ya kuanzisha vyanzo vipya vya mapato vya Halmashauri badala ya kuwa na mawazo ya kutegemea vyanzo ambavyo vinaweza kufikia ukomo wakati wowote.
Akizungumza katika kikao kazi maalumu kilichojumuisha Viongozi na Watendaji kutoka Wilaya ya Njombe Mtaka amesema kuwa Halmashauri zimeshindwa kuwekeza kwenye mawazo ya kibunifu na kuwa na vyanzo vya kiuwekezaji na hivyo kushindwa kuongeza mapato maradufu ya mapato yanayokusanywa sasa.
"Zipo Halmashauri ambazo zimeanzisha miradi ya kiuwekezaji kama hoteli, kumbi za sherehe, mikutano, uwekezaji kwenye Ardhi,Viwanda.Ni vyema kujifunza kwa wenzetu na kuona wao wamefanya nini ili na sisi tuweze kuwa na ukusanyaji wenye tija badala ya kutegemea makusanyo ambayo muda wowote chanzo unachokusanya kinaweza kisiwepo na hivyo kukusababishia kukosa mapato"Alisema Mtaka
Mtaka aliendelea kusema kuwa suala la kuongeza ukusanyaji mapato limekua ni jambo la kawaida lakini kwa sasa timu za kitaalamu za halmashauri na kamati za fedha na mabaraza ya Madiwani inabidi kubadilika na kuja na mitazamo mipya ya kuongeza marambili thamani ya makusanyo yaliyokuwa yanakusanywa kwenye Halmashauri awali.
Akichangia hoja katika kikao Kazi hicho Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Njombe Erasto Mpete amesema kuwa Halmashauri ya Mji Njombe inamipango ya kufanya uwekezaji wenye tija na tayari ipo katika mipango ya kuwa na maeneo ya maegesho ya malori, kumbi za sherehe, Ujenzi wa Shule za kisasa za mchepuo wa kiingereza ili kuweza kuwa na vyanzo vya kudumu kwenye ukusanyaji mapato.
Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Mji Njombe kimehusisha Wenyeviti wa Halmashauri, Madiwani, Wakurugenzi, Wenyeviti wa Vijiji na Mitaa,Maafisa Tarafa,Watendaji wa Vijiji na Mitaa na Viongozi mbalimbali wote kutoka Wilaya ya Njombe
Ofisi yetu inapatikana barabara ya Njombe-Songea mtaa wa Mjimwema.
Sanduku la Posta: S.L.P 577
Simu ya Mezani: 026-2968833
Simu ya Mkononi: 026-2968833
Barua Pepe: td@njombetc.go.tz
Haki Miliki ©2017 Halmashauri ya Mji Njombe