Wazazi na walezi katika kijiji cha Luponde Halmashauri ya Mji Njombe ,wametakiwa kuzingatia elimu ya lishe inayotolewa kwa kutenga muda wa kuwahudumia watoto wao licha ya kujikita kwenye shughuli za kujitafutia kipato.
Wito huo umetolewa Mei 28,2024 na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Njombe Bi.Kuruthum Sadick kwenye Siku ya Afya na Lishe ya kijiji (SALIKI) iliyofanyika katika kijiji cha Luponde.
“Tujitahidi kuwa na muda kamili wa kuwa hudumia watoto,tukifundishwa tukayachukua halafu tusiyazingatie itakuwa ni kazi bure, kazi tufanye lakini tupate muda wa kuhudumia watoto,niwaombe wamama wa Njombe, ninaelewa ni watafutaji kwelikweli,asubuhi kabla hujaenda shamba hakikisha unamuandalia mtoto wako lishe iliyo bora.”Alisema Bi.Kuruthum,Mkurugenzi Njombe Mji.
Aidha amesema ili kuondokana na vitendo vya ukatili kwa watoto ni lazima mama kuwa na muda wa kuzungumza na watoto wake sambamba na kuwachunguza.
“Licha yakuwalisha watoto tunaona vitendo vibaya vinafanyika kwa watoto,mnashuhudia wenyewe watoto wanabakwa, watoto wananajisiwa ,hii ni kwa sababu wamama tumewaacha watoto wetu hatuna muda nao,mtoto akitoka shule muangalie,muulize huko shuleni leo imekuwaje ,sisi wa mama ndiyo tunatunza familia ,sidhani kama kuna mama anataka kitu kibaya kitokee kwa mtoto wake”.Alisisitiza Bi.Kuruthum
Katika hatua hatua nyingine amewaomba wazazi waliopatiwa elimu kufikisha elimu hiyo kwa waume zao na wazazi wengine sambamba nakuhakikisha wanakuwa na bustani ya mbogamboga nyumbani ili kuwa na uhakika wa upatikanaji wa kundi la mbogamboga kwenye mlo wa familia.
Ili kufanikisha hilo amemtaka Mtendaji na Afisa kilimo wa kata ya Luponde kushirikiana na uongozi wa kijiji kutoa elimu ya bustani jiko ili jamii yote ihamasike kupanda mbogamboga nyumbani.
Hali ya udumavu katika Halmashauri ya Mji Njombe imepungua kwa asilimia 3 kutoka 45% Disemba 2022 hadi 42% mwaka 2024.
Ofisi yetu inapatikana barabara ya Njombe-Songea mtaa wa Mjimwema.
Sanduku la Posta: S.L.P 577
Simu ya Mezani: 026-2968833
Simu ya Mkononi: 026-2968833
Barua Pepe: td@njombetc.go.tz
Haki Miliki ©2017 Halmashauri ya Mji Njombe