Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Njombe Ndugu Kuruthum Sadick, ametoa wito kwa wazazi na walezi wanaoishi na watoto wenye mahitaji maalum kuhakikisha wanawapeleka watoto hao kwenye shule maalumu zilizotengwa.
Ndugu Kuruthum ametoa rai hiyo Oktoba 25,2023 wakati akikabidhi kiti mwendo kwa mtoto mlemavu mkazi wa kata ya Ramadhani Halmashauri ya Mji Njombe.
"Mama mtoto huyu mpeleke shule atapata kitu cha ziada akikutana na wenzake, pale kibena si umekwenda nakuona wengine huyu pia anastahili nafasi hiyo. "Alisema Ndugu Kuruthum Sadick.
Kwa upande wake mganga mkuu wa Halmashauri ya Mji Njombe Daktari Jabir Juma, ametoa msisitizo kwa walezi wa mtoto huyo endapo kutakuwa na changamoto kuendelea kuwasiliana na ofisi ya Mkurugenzi kupitia Ustawi wa Jamii ili waweze kupatiwa ushauri na msaada zaidi.
" Msikae kimya kwa jambo lolote wasiliana na afisa ustawi, ofisi ipo wazi Msikae kimya"Alisema Mganga mkuu.
Kwa upande wake afisa ustawi wa Jamii wa Halmashauri ya Mji Njombe Petro Mahanza amekemea vikali tabia ya baadhi ya wazazi na walezi kuwaficha watoto wenye mahitaji maalumu kwani wanawanyima fursa yakupata haki zao za msingi.
"Msiwafiche wenye ulemavu, tuwaibue ili wapate haki, ofisi yetu ipo wazi kwa ajili yakushughulikia changamoto hasa za watu wenye mahitaji maalum." Alisema Petro mahanza.
Akizungumza kwa niaba ya Familia Ndugu Tito Mpangale amemshukuru Mkurugenzi kwa kuona umuhimu wakuwasaidi wahitaji.
" Kiti mwendo hiki kinaenda kuwa msaada mkubwa sana, tulikuwa tunapata changamoto hasa tulipohitaji kumtoa nje.
Kitimwendo hicho kimenunuliwa kwa fedha za mapato ya ndani ya Halmashauri ya Mji Njombe.