Mei 30, 2025 Watumishi wa dini kutoka madhehebu mbalimbali, wakiongozwa na Mchungaji Nelson Godiwe, wameungana kwa pamoja katika ibada maalum ya kuwaombea watumishi wa Halmashauri ya Mji Njombe.
Ibada hiyo imefanyika katika ukumbi wa Halmashauri ya Mji Njombe, ikiwa na lengo la kuwaombea watumishi hao amani, mshikamano, upendo, umoja na mafanikio katika utekelezaji wa shughuli za maendeleo kwa manufaa ya wananchi.
Akizungumza katika hafla hiyo, Mchungaji Nelson Godiwe kutoka Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) alisema kuwa sala na dua ni nguzo muhimu katika kuhakikisha mazingira ya kazi yanabaki kuwa ya utulivu na yenye maadili ambapo alisisitiza kuwa viongozi wa umma wanapaswa kuwa mstari wa mbele katika kuomba baraka za Mungu kwa ajili ya kazi zao.
“Watumishi wa serikali ni mihimili muhimu ya maendeleo ya taifa, maombi haya ni muhimu ili kuwajengea msingi wa maadili, upendo na uaminifu katika utendaji wenu wa kila siku,” alisema Mchungaji Godiwe.
Kwa upande wake, Shehe Rajabu Msigwa alieleza kuwa mafanikio ya taifa lolote yanatokana na mshikamano na upendo miongoni mwa wananchi wake ambapo ushirikiano kati ya viongozi wa serikali na wananchi unapaswa kuimarishwa kupitia misingi ya heshima na maadili ya kidini.
Naye Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Njombe, Bi. Kuruthum Sadick katika salamu zake kwa washiriki wa ibada hiyo, alikumbusha kuwa uzima na mafanikio hutoka kwa Mungu ambapo alisema kuwa ni wajibu wa kila mtumishi wa umma kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na moyo wa kujitolea, kwa kuwa wanahudumia wananchi na taifa kwa ujumla.
Ibada hiyo imeonyesha mshikamano wa kiroho kati ya viongozi wa dini na watumishi wa serikali, ikiwa ni hatua ya kuimarisha maadili na kuongeza moyo wa uzalendo na uwajibikaji katika utumishi wa umma.
Ofisi yetu inapatikana barabara ya Njombe-Songea mtaa wa Mjimwema.
Sanduku la Posta: S.L.P 577
Simu ya Mezani: 026-2968833
Simu ya Mkononi: 026-2968833
Barua Pepe: td@njombetc.go.tz
Haki Miliki ©2017 Halmashauri ya Mji Njombe