Akielezea madhumuni ya mafunzo ya ulishaji samaki kwa wafugaji, Daktari Gloria Yona ambaye ni Mtafiti Mwandamizi wa maswala ya Samaki amesema kuwa mafunzo hayo yamelenga katika kumsaidia Mfugaji wa hali ya chini kuweza kumudu gharama za chakula kwa kutumia malighafi zinazomzunguka na kuepuka matumizi ya vyakula vya madukani ambavyo vimekuwa ni vya gharama kubwa.
Baadhi ya wafugaji samaki waliopata mafunzo hayo akiwemo Emmanuel Kinyamagoha, Theodori Mlowe wamesema kuwa mafunzo hayo yamekuwa ni ya manufaa kwao kwani zoezi la ulishaji samaki lilikuwa ni changamoto kubwa iliyokuwa inawakabili jambo lililokuwa likipeleka kutumia fedha nyingi kununua vyakula vya samaki kwenye maduka na bila kuzingatia utaalamu wa uchanganyaji chakula wakati wa ulishaji.
“Shida kubwa ilikuwa ni upatikanaji wa elimu. Watu wengi katika Mkoa wetu wanahamasika kufanya shughuli za ufugaji samaki. Tuchangamkie fursa hii kwani pia si kutuongezea kipato tuu bali kusaidia kupunguza tatizo la udumavu unaoukabili Mkoa wetu wa Njombe.”Alisema Lupenza mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo.
Awali akifungua mafunzo hayo Katibu Tawala Wilaya ya Njombe George Emmanuel amesema kuwa ni vyema kuitumia fursa hiyo ya mafunzo ipasavyo kwani itasaidia katika kuleta maendeleo ya mtu mmoja mmoja na hivyo kuendeleza mnyororo wa thamani.
“Niwaombe Watendaji kuhakikisha kuwa baada ya mafunzo haya ufuatiliaji unafanyika kwa wafugaji wa samaki ili kuweza kutatua changamoto zitakazokuwa zinawakabili” Alisema Katibu Tawala.
Licha ya kuwepo kwa hamasa kubwa ya ufugaji samaki katika Halmashauri ya Mji Njombe, changamoto kubwa imekuwa ni wafugaji wengi kutowahusisha wataalamu wa mifugo ili kuweza kupata ushauri wa Kitaalamu jambo ambalo limepeleka wafugaji wengi kufanya ufugaji wa mazoea na hata wakati mwingine kuingia gharama nyingi katika kununua vifaranga vya samaki.
Ofisi yetu inapatikana barabara ya Njombe-Songea mtaa wa Mjimwema.
Sanduku la Posta: S.L.P 577
Simu ya Mezani: 026-2968833
Simu ya Mkononi: 026-2968833
Barua Pepe: td@njombetc.go.tz
Haki Miliki ©2017 Halmashauri ya Mji Njombe